Uwezekano wa kupatikana mkataba wa amani mwaka huu mashariki mwa Jamhuri
ya Kidemokrasia ya Kongo umeonekana kila mara kuwa finyu. Mapigano
mapya ya wiki iliyopita yamedidimiza zaidi matumaini.
Duru mpya za mapigano katika wiki iliyopita kati ya jeshi la Kongo na
kundi la waasi wa M23 yamezidi kukatisha matumaini ya kupatikana
makubaliano ya aina yoyote. Kwa sasa kila upande hauonekani kuwa tayari
kukubali maridhiano ya kufikiwa kwa mkataba. Lakini kuna dalili kwamba
jeshi la Kongo linaanza kuwa na nguvu zaidi kuliko kundi la M23 jambo
ambalo wachambuzi wanasema ni ishara ya kutia matumaini.Msaada zaidi wa jeshi la Kongo unatoka kwa Umoja wa Mataifa, ambao unasema brigedi yake ya mapambano, ya kwanza kuwahi kupewa mamlaka ya kuyachakaza makundi ya waasi, ina wanajeshi takriban 2,000 walio tayari. Kwa sasa kiasi thuluthi mbili ya kikosi cha kimataifa kiko katika uwanja wa mapambano, amesema Madnodje Maounoubai, msemaji wa kikosi cha Umoja wa Mataifa cha kulinda amani nchini Kongo, MONUSCO.
Waasi wa kundi la M23
Msaada wa Umoja wa Mataifa unatakiwa kuongeza kasi na uzito kwa jitihada
za kuimarisha mamlaka zaidi katika maeneo ambayo kwa kiwango kikubwa
yamekuwa yakidhibitiwa na waasi kwa karibu miongo miwili. Kundi la M23
lililoanzishwa mwaka 2012 na wanajeshi waasi, wengi wao wa kabila la
Tutsi, limeifanya vigumu azma hiyo kufikiwa. Vikosi vyake viliuteka mji
wa Goma mwezi Novemba mwaka jana. Tukio hilo la aibu la kushindwa kwa
jeshi la Kongo, liliilazimu serikali ya mjini Kinshasa kushiriki
mazungumzo ya kutafuta amani mjini Kampala nchini Uganda. M23 ilikuwa na
furaha kushiriki mazungumzo hayo, kwa kuwa iliamini ilikuwa ikipata
kutambuliwa kisiasa na kudai ilichokuwa ikikitaka ikiwa na nafasi imara
kwenye mashauriano hayo.Mambo yamebadilika
Lakini miezi kadhaa baadaye, mambo yamebadilika kabisa. Jeshi la Kongo limeimarisha uwezo wake ikiwa ni pamoja na kuhakikisha mishahara ya wanajeshi inalipwa bila kuchelewa, na kuwapa silaha na risasi wanajeshi walio katika uwanja wa mapambano. Jeshi hilo pia limefaulu kuwahamisha wanajeshi mafisadi katika maeneo mengine yaliyo na utulivu katika taifa hilo lenye wakazi milioni 72.
Jason Stearns, mchambuzi wa masuala ya Kongo, anasema huku matatizo ya jeshi la Kongo yakiwa bado yako mbali mno kupatiwa ufumbuzi, mazungumzo na maafisa wa Umoja wa Mataifa na makamanda wa jeshi yanaashiria jeshi limekuwa imara zaidi kiasi cha kuwa kikosi bora cha mapambano vitani. Kwa mujibu wa Stearns, jeshi bado linakabiliwa na changamoto tatu kubwa zikiwemo ulezi, utapeli na kufanya makosa bila kuwa na hofu ya kuadhibiwa wala kuchukuliwa hatua yoyote kisheria.
Bosco Ntaganda, alipohudhuria harusi ya kamanda Sultani Makenga, Goma 27.12 2009.
Kwa upande mwingine mivutano ya ndani ililidhoofisha kundi la
M23 na kusababisha mpasuko katika uongozi wake. Mmoja wa waasisi wa
kundi hilo, Bosco Ntaganda, alipata hasara kubwa katika vita hivyo vya
ndani na akalazimika kujisalimisha mwenyewe katika mahakama ya kimataifa
ya uhalifu, ICC, mjini The Hague, Uholanzi, ambako anasubiri kesi ya
mashtaka ya uhalifu wa kivita. Kwa wakati huo huo Rwanda, taifa
linalotuhumiwa kwa kulisaidia kundi la M23, ilikabiliwa na vikwazo
kutoka kwa mataifa ya magharibi.Kwa sasa serikali ya mjini Kigali iko katika mtanziko, anasema Thiery Vircoulon, mchambuzi katika shirika la kimataifa linaloshughulikia mizozo, ICG. "Kama hawataiunga mkono M23 basi M23 itafukuzwa kutoka Kongo na jeshi la Kongo. Kama wataliunga mkono kundi hilo, watakuwa chini ya uchunguzi na huenda wakakabiliwa na vikwazo."
Mazungumzo ya Kampala shaghala bagala
Nchini Uganda, mazungumzo yamekuwa yakifanyika bila mpango, wakati wapatanishi wanapojali na kuhudhuria. Daniel Bekele wa shirika la kutetea haki za binaadamu la Human Rights Watch tawi la Afrika, anasema Rwanda inabakia kuliunga mkono kundi la M23 kwa maana kwamba itaendelea kufanya hivyo kwa muda mrefu.
Vircoulon na wachanganuzi wengine wanasema hali hii inaibua hofu kuwa kuna vivutio vichache sana kwa lengo la kuzingatia kwa bidii mazungumzo ya amani. Serikali ya Kongo inaweza pia kusita kuyakubali maridhiano kwa matumaini kwamba jeshi lake, kupitia msaada wa Umoja wa Mataifa, litaendelea kuyakomboa maeneo yanayodhibitiwa na waasi. Hadi sasa imekuwa ikiwatuma wajumbe wa ngazi ya chini katika mazungumzo ya Kampala. Hivyo, wachambuzi wanasema shinikizo jipya kutoka jeshini linapunguza uwezekano wa kuongezeka kwa machafuko, lakini halifai kwa mazungumzo ya amani.
0 MAONI :
Post a Comment