Enzi ya kusubiri yamalizika Waingereza waamka leo(07.07.2013)wakiwa
mabingwa wa tennis wa Wimbledon baada ya kusubiri miaka 77. Muingereza
Andy Murray awa shujaa wa Uingereza baada ya kumwangusha Novak Djokovic.
Sauti zilipazwa, na shangwe zilikuwa zinaongezeka kila wakati, kila
point iliyokuwa inapatikana ambayo ilikuwa inamchukua Andy Murray karibu
na kumaliza miaka 77 ya Uingereza kusubiri kulinyakua taji la
Wimbledon.Ndiyo hali inayoweza kuelezewa katika mchezo wa tennis uliofanyika jana kati ya Andy Murray wa Uingereza na Novak Djokovic wa Serbia , ambapo mashabiki 15,000 walishuhudia patashika nguo kuchanika katika fainali iliyodumu karibu saa tatu na nusu na hatimaye kwa mara ya kwanza katika muda wa
miaka 77 Uingereza umeweza kuonja raha ya kuwa mabingwa tena katika mchezo huo.
Mafanikio ya Grand slam hayakuja kirahisi ana haraka kwa Andy Murray katika muda wake wa kucheza tennis, na hakika hayakuja kwa haraka Uingereza katika uwanja wao wenye sifa tele na pia mashindano hayo maarufu duniani ya Wimbledon. Kwa hiyo kulikuwa na kitu kinachoendana na mchezo huo jana , hamasa ikiongezeka, wasi wasi , shauku na kila aina ya mvuto kwa Waingereza kusubiri muda zaidi kuweza kutawazwa mabingwa wa taji hilo.
Andy Murray ambaye yuko katika nafasi ya pili katika orodha ya wachezaji bora wa mchezo wa tennis duniani kwa wanaume, amemshinda mchezaji nambari moja Novak Djokovic kwa seti 3-0 , kwa michezo 6-4 , 7-5 na 6-4.
Andy Murray amesema haikuwa rahisi kama ilivyoonekana:
"Nilifanyakazi ya ziada katika mchezo ule. Ni points chache ambazo nimezipata kwa taabu sana katika mchezo kama huo katika maisha yangu. Ulikuwa mchezo tofauti kabisa ukilinganisha na mashindamno ya US open na kushinda ubingwa wa Wimbledon. Ndio ... kwa kweli bado sijaamini, nashindwa kuweka kichwa changu sawa nikifikiri kuhusu mchezo huo. Siamini."
Naye Novak Djoklovic alimwagia sifa tele Murray kwa ushindi wake jana.
"Ukweli ni kwamba alicheza vizuri sana katika wakati muafaka. Nilikuwa katika seti ya pili na ya tatu , mbele kwa 4-2 na kupoteza mipira ya kuanzia katika mchezo huo na nilimruhusu kunipita bila sababu maalum. Alipata ushindi katika kila mchezo na alikimbilia kila mpira na kuupata. Alikuwa kila mahali katika eneo lake na alionesha mchezo wa hali ya juu wa tennis. Bila shaka yoyote, alistahili kushinda."
Baadhi ya mashabiki wa mchezo huo wanasema kuwa mchezo wa tennis sasa unarejea katika hadhi yake na shauku, baada ya kudorora kidogo.
Jumamosi Wajerumani walikuwa katika runinga zao wakikodolea macho mchezo wa tennis kati ya kijana chipukizi Sabine Lisicki na Marion Bartoli wa Ufaransa : Katika mchezo huo Marion Bartoli aliibuka mshindi kwa seti 2-0 , kwa michezo 6-1 na 6-4.
Nao Daniel Nestor na Kristina Mladenovic waliibuka kidedea baada ya kushinda pambano dhidi ya Bruno Soares na Lisa Raymond kwa seti 2-1 kwa michezo 5-7 6-2 na 8-7 kwa wachezaji wawili wawili wanaume na wanawake jana katika mashindano hayo ya Wimbledon.
0 MAONI :
Post a Comment