Shirika la kimataifa la kutoa msaada la madaktari wasio na mipaka Medicins Sans Frontieres limesema, watu takriban 355 wameuwawa wiki iliopita nchini Syria kutokana na mashambulizi ya gesi ya sumu. Shirika hilo limesema pia zaidi ya watu 3000 mjini Damscus walionesha dalili za kuathirika na gesi hiyo.
Shambulio la siku ya Jumatano linalodaiwa kuwa ni gesi ya sumu lililosababisha mamia ya watu kufariki wakiwemo watoto liliongeza wasiwasi kwa jumuiya ya Kimataifa na kuanza mazungumzo ya hatua ya haraka itakayochukuliwa dhidi ya nchi hiyo. Afisa wa ngazi ya juu wa Umoja wa Mataifa Angela Kane yuko mjini Damascus kuishinikiza serikali ya Syria kuwaruhusu wachunguzi wa Umoja huo kufanya uchunguzi katika maeneo yanayodaiwa kutumika kemikali za sumu.Kansela wa Ujerumani Angela Merkel pia ametaka wachunguzi wa Umoja wa Mataifa kuruhusiwa kuingia katika maeneo hayo mara moja.Rais wa Marekani Barrack Obama anatarajiwa kukutana na washauri wake wakuu juu ya swala hilo huku Jordan ikipanga kufanya mkutano juu ya Syria wiki hii mjini Amman.

0 MAONI :
Post a Comment