MTUNZI:JAPHET NYANG'ORO
“Jacob napenda kuolewa ila haiwezekani” Alisema ili hali mikono yake ikiwa bado inaminya minya misuli ya mwanaume huyu huku pia machozi yakiwa yanamtiririka.
“Kwa nini ishindikane Regina ili hali wewe ni msichana ambaye unaweza kumvutia kila mwanaume mwenye mpango wa kupata mwenza wa maisha? Jacob aliuliza huku akihisi ubaridi uluokuwa ukipenya taratibu katika kifua chake, kutokana na machozi yaliyokuwa yakitoka kwa wingi machoni kwa Regina.
“Hapana haiwezekani Jacob…” Regina alisisistiza kwa sauti ya taratibu, iliyoonyesha huba na wasiwasi.
"Usiseme hivyo Regina!
"Hata nisiposema huo ndiyo ukweli na hali halisi Jacob"
“Naomba sababu ya huko kutowezekana…” Jacob alizidi kuhoji kwa shahuku.
"Hata nikikwambia huwezi badili hali na ukweli wa mambo"
"Umejuaje kama sitoweza?
"Uko peke yako wako jeshi, huwezi washinda wote....ni waovu sana!
"Nakupenda Regina, niko tayari kufanya lolote ili kurejesha uhuru wako na amani" maneno hayo ya Jacob ilikuwa kama sauti ya muziki mororo inayopenya kwenye kiza kinene na kuyafikia masikio mtu aliyenyeshewa na mvua nzito.
"Sijawahi kuwa huru na sijui amani ikoje Jacob" alisema Regina huku akimkazia macho Jacob, kamasi nyembamba na machozi vikiendelea kuchuruzika.
Wakati mahojiano hayo yakiendelea, sauti yake Bella wa Akudo Impact ilikuwa ikivuma ukumbini hapo huku yale mashairi ya wimbo wake ‘yako wapi mapenzi? ilimfanya kila aliyekuwepo kujishughulisha zaidi na mwandani aliyekuwa naye. Kwa kifupi hali ilikuwa ni ya kuvutia na utulivu katika ukumbi wa Miami Hoteli ambayo ni moja kati ya hoteli za kuvutia zilizoko kando kidogo ya jiji la Dar es salaam baada ya kupita mbezi beach.
Ni kawaida kwa Jacob Matata kutoka nyakati za jioni na kwenda katika mojawapo ya maeneo ya burudani katika jiji la Dar es salaam. ukimuuliza mwenyewe kwa nini alipenda kwenda maeneo hayo, sababu nyingi angekupa. Lakini katika orodha yake asingesita kutaja, upweke, burudani na kusafisha macho. Lakini ana jingine ambalo kamwe usingelisikia akilitaja...........kazi....ka
Siku hiyo Jacob Matata alijikuta anavutiwa kwenda Miami hoteli. Alisikia Akudo Impact wanapiga huko na kwa vile yeye ni mpenzi wa muziki wao akaona ni bora akaishibishe nafsi yake kitu inataka. Binafsi anamiliki magari mawili, lakini hakuwa anapenda kwenda sehemu za starehe akiwa anaendesha, hivyo alimtaarifu Abdul mmoja wa vijana wake ambao hupenda kuwakodisha akiwa kwenye mizunguko yake na wakati akiwa hataki kuendesha. Abdul alimpitia Jacob nyumbani kwake maeneo ya Sinza Mori mida ya saa tanu unusu usiku.
“vipi bosi, naona leo umekaa kiburudani Zaidi? Abdul alimwambia Jacobn ambaye alikuwa amevaa fulana ya blue na suluali ya jeans nyeusi.
“Si unajua wazee wa masauti Akudo wako Miami Hotel, sasa nataka nikakate kiu huko” Jacob alisema
“Ahhh wale jamaa nawakubali sana hata miye” Abdul alijibu.
Saa nne na robo ilimkuta Jacob ameshatulia kitini katika Ukumbi wa hoteli ya Miami. Akudo walikuwa wameshaanza kushambulia jukwaa taratibu. Alitafuta sehemu na kukaa, kabla ya kuagiza aletewe vinywaji. Vinywaji vililetwa na taratibu akaanza kujipigilia huku akiyapa fursa macho yake yaweze kutalii katika ukumbi mpana wa hoteli hiyo...kusafisha macho. Jacob aliamua aweke mbili tatu ili wakati mambo yakichanganya naye awe kamili. Tangu alipoingia hotelini hapo, Jacob Matata alionekana kuwa mtulivu japo utulivu ni hali ya kujifunza tu kwake, asili yake ni mtu mchangamfu sana na mtundu unaweza sema. Hata ukienda mitaa aliyokulia pale Mwanza mjini maeneo ya Kirumba mwaloni, ambapo nyumba ambayo wazazi wake walikuwa wamepanga ilikuwa jirani na msikiti wa Taqwa, siku hizi kuna shule ya sekondari ya kiislamu pale, ukiuliza utaambiwa wakati Jacob anakuwa miaka ile ya 1991, wazazi walikuwa wakiwazuia watoto wao wasicheze pamoja naye. Alikuwa mtundu balaa.
.
Kadiri masaa yalivyokuwa yakizidi kukatika, ndivyo ukumbi huo ulivyokuwa ukipungua watu. Pamoja na kuwa kulikawa na watu wengi wa rika na maumbile tofauti, lakini macho ya Jacob Matata yaligota kwa msichana mmoja aliyekuwa ametulia tuli juu ya kiti upande wa kulia wa ukumbi huo. Alipozidi kumtazama Jacob aliweza kubaini uzuri wa msichana huyo. Hivyo mara kwa mara macho yake yakawa yanapendelea kuangalia upande alipokuwa amekaa kiumbe huyo wa kike. Dakika kumi baadae Jacob alitupia macho kwa yule msichana mrembo na kubaini kuwa hakuwepo sehemu ile aliyokuwa amekaa. Wakati anageuza macho katika jitihada za kujaribu kuangaza ili aweze kuona kama bado msichana huyo alikuwepo ukumbini hapo, ndio macho yake yalipogongana moja kwa moja na yale ya msichana mrembo akiwa amekaa hatua chache tu kwa nyuma yake. Macho yao yalipogongana, yule msichana aliachia tabasamu la kukaribisha. Kuona hivyo, Jacob aliachia lake la mwitikio na kusita kidogo. Aliangalia saa yake ya mkononi na kubaini kuwa tayari ilikuwa inaelekea kuwa saa tano na robo usiku. Jacob alisimama, kabla ya kupiga hatua yoyote alizungusha macho yake huku na huko ili kuona kama kulikuwa na lolote, alipooona hakuna aligeuka na kuanza kuelekea alipokuwa amekaa yule mrembo.
Haikuwachukua muda mrefu wakajikuta wameshatambulishana. Muda si muda wakakubaliana kumalizia muda uliobaki kwa kucheza muziki pamoja.Na wakati huo ule wimbo maarufu wa ‘yako wapi mapenzi? ulikuwa ukiimbwa kwa ustadi mkubwa nae Bella. Haikuwa siri kuwa kila mmoja katika watu hawa alikuwa amevutiwa na mwenzie.
Sijui kama ndiyo ilikuwa kosa au la, pale Jacob alipomwuliza msichana huyu kama alikuwa na mtu yeyote. Jibu alilolipata lilikuwa ni lile ambalo Jacob alikuwa anaombea apewe. Kule kusikia kuwa Regina hakuwa na mtu kulimfurahisha sana Jacob. Hapo ndipo akauliza swali la kichokozi na ambalo hata hivyo ndilo liloleta kizaa zaa kinachoendelea.
Wakati huu walikuwa bado wamekumbatiana katika hali ya mapenzi huku Jacob akiwa anasisitiza kutaka kujua sababu ya mrembo huyu, aliyejitambulisha kama Regina kusema kuwa haiwezekani yeye kuolewa.
“Kweli haitawezekana, hata kitendo cha mimi kukumbatiana na wewe kiasi hiki ni ujasiri tu nilio nao. Haikutakiwa mimi nikukumbatie kiasi hiki, nimeshindwa kujizuia Jacob nimeshindwa...............umen
“Hapana Regina kabla haujaondoka naomba unijulishe tatizo lako, kwani siamini kuwa swali langu ndilo lilosababisha wewe utokwe na machozi mengi kiasi hiki. Isitoshe niko tayari kukusaidia kwa namna yoyote ile kama nitaweza” Jacob alisema huku akizidi kumvuta Regina ili atulie zaidi katika kifua chake.
“Jacob nakuonea huruma sana kwani hata hapa tu najua maisha yako yatakuwa mashakani” Alisema Regina huku akiinua Kichwa chake na kuangaza hapa na pale ukumbini hapo.
“Hatarini kivipi Regina? Mbona sikuelewi?
“Kuna watu Jacob, watu wasiotaka niolewe kwa faida yao. Kama ni kuolewa basi inamaanisha kifo chang………” Kabla Regina hajamalizia, Jacob alishitukia anapigwa na kitu kizito kisogoni na papo hapo akajikuta anapoteza uwezo wa kupambanua mambo, hata mashairi ya wimbo wa ‘safari siyo kifo’ wa Akudo Impact akawa anasikia yakipotelea hewani, akapoteza fahamu na hivyo kutojua ni nini kilikuwa kinaendelea.
*****
Aliporejewa na fahamu alijikuta yuko amelazwa kwenye kitanda. Pembeni yake alikuwa amekaa msichana mrembo akiwa amevalia kiuguzi.
“Habari yako binti mrembo? Jacob alisema kwa sauti dhaifu kidogo.
“Afadhali....aaaaaaaanha!!!! Alisema msichana huyo huku akishusha pumzi ndefu na mikono yake yote miwili akiwa kaiweka juu. Tendo hili ilikuwa ni ishara tosha kuwa msichana huyu alikuwa anangojea kusikia sauti hii ya Jacob kwa hamu kubwa. Baada ya kutoa ukelele huo wa furaha msichana huyu alisimama na kukisogelea kitanda ambacho Jacob alikuwa amelalia.
Jacob alimwangalia Msichana huyu bila kusema neno jingine zaidi ya ile salamu aliyokuwa ameitoa mwanzo. Hapo tena zilipita kama dakika mbili watu hawa wawili ndani ya chumba wakiwa bado wanaangaliana tu bila kusema neno. Jacob alikuwa na hamu ya kujua msichana ambaye alikuwa ameshindwa kabisa kuficha furaha aliyokuwa nayo kuona Jacob amerejew na fahamu.
Baadae Jacob akapata wazo la kuangalia saa yake. “saa kumi!! Jacob alinong’ona kwa sauti ambayo iliweza kuyafikia masikio ya msichana.
“Ndiyo, pole sana kaka yangu” Hatimaye binti huyo alisema huku akipitisha mkono wake kifuani kwa Jacob katika ile hali ya muuguzi kumjulia hali mgonjwa.
“Pole kwa lipi” Jacob aliuliza kana kwamba hakuwa anajua nini kilikuwa kikiendelea.
“Najua huwezi kujua. Kwa kifupi ni kuwa jana wakati ulipokuwa ukicheza muziki na msichana fulani, Miami hoteli, alitokea kijana mmoja na kukupiga na kitu kichwani ukaanguka chini. Yule msichana uliyekuwa ukicheza naye alipojaribu kukutetea naye alipigwa kablwa ya kubebwa na vijana wengine ambao bila shaka walikuwa na yule aliyekupiga. Watu hao wakatokomea wakiwa wamemchukua yule msichana huku wewe ukiwa umeachwa pale chini bila msaada. Baada ya tukio hilo, hali ndani ya ukumbi haikuwa shwari tena. Watu walianza kukimbia hovyo, hakuna hata mmoja aliyejitokeza kukupa msaada. Miye ni muuguzi, najua kuwa kama ungekaa mazingira yale bila msaada ungeweza kupoteza maisha kabla ya siku zako, hivyo nikaamua kukuchukua. Tangu jana nilipokuleta hapa hujarudiwa na fahamu mpaka sasa hivi. Nilianza kudhani kuwa umefariki” Alimaliza msichana huyo ambaye hakuweza kuficha furaha yake.
“Asante sana kwa kukubali kuwa mkombozi wangu” Jacob alipomwangalia msichana huyo aliona kitu katika macho yake japo hakujua kwa haraka kilikuwa nini. Alijiinua pale kitandani, akaketi. Akatembeza macho katika chumba hicho alichokuwa amelazwa. Jambo moja alitambua ni kuwa chumba hiki kilionekana kuwa maalumu kwa kazi kama hii aliyokuwa amefanyiwa.
“Je hapa ni hospitalini? Hatimaye Jacob alimwuliza yule msichana ambaye alikuwa amekaa pembeni yake kana kwamba anayasoma mawazo yake.
“Hapana” alijibu
“Kwa hivyo ni wapi hapa?
“Hapa ni nyumbani kwangu”
“Unataka kuniambia kuwa ulijua kuwa utakutana na mkasa kama huu mpaka ukawa umejiandaa kiasi hiki katika chumba hiki?
“ Hapana ila huwa na…” alisita kabla ya kuendelea “…mimi ni nesi hivyo huwa natunza chumba hiki hapa kwangu kwa ajili ya kuwasaidia ndugu na jamaa pale inapobidi” Alisema msichana huyo katika sauti iliyokuwa na shaka.
“Asante sana” Jacob alisema huku akijaribu kujinyoosha. Alihisi kichwa chake kizito. Hii ilitokana na pigo alilokuwa amelipata.
“Naomba twende nikuonyeshe bafu ili uoge kisha upate chochote, maana ni masaa mengi yamepita hivyo nina hakika una njaa” Alisema msichana huyo huku akiwa anaanza kupiga hatua kuelekea mlango wa kutokea katika chumba hicho. Jacob akaanza kumfuata bila wasiwasi wowote.
Walipita vyumba kadhaa kabla ya kutokezea sehemu iliyooneka kuwa ni maalumu kwa shughuli za usafi.
“Huo mlango ndiyo bafu, kuna kila kitu kwa shughuli ya uogaji. Naomba ujisikie huru kaka” Alisema huku akiwa amesimamana kumwangalia Jacob akitokomea bafuni.
Baada ya kuoga na kupata huduma nyingine zilizotakiwa baada ya kuoga, tayari kulikuwa kumeshaanza kupambazuka vizuri. Baadaye Jacob alikaribishwa sehemu aliyoambiwa kuwa ilikuwa maalumu kwa chakula. “Kama nilivyotangulia kusema jisikie huru na usiwe na wasiwasi” Alisema msichana huyu ambaye mpaka hapo hakuwa anajua Jacob Matata alikuwa ni mtu wa namna gani.
“Nafikiri tutumie fursa hii kwa ajili ya kujuana pia” Jacob alisema wakati wakiwa wameshaanza kupata kifungua kinywa.
“Naona umeniwahi kusema, kwani nami nilikuwa nikiwaza hivyo” alisema msichana huyo ambaye kwa kila namna alionekana kufurahia sana kuwepo kwa Jacob mahali hapo, kisha akaendelea “Mimi kwa jina naitwa Evelyn, wachache wanaonifahamu huniita Eve. Ni nesi katika hospitali moja binafsi hapa jijini. Naipenda kazi yangu kwani inanitosheleza na kunifanya niishi hapa mjini. Nadhani mpaka hapo inatosha” Alisema msichana huyo huku akiwa kayatuliza macho yake kwenye mikono yake. Jacob alijikuta yuko katikati kati ya kumwamini na kumwelewa au kumtilia shaka na kutaka kumfahamu zaidi msichana huyu. Hata pale alipoulizwa na Eve juu ya jina lake Jacob alijikuta anapingana na nafsi yake juu ya nini amwambie.
“Aah naitwa Nico Mkenja, ni mfanyabiashara” Jacob alidanganya huku uso wake ukiachia tabasamu liloonyesha kuwa aliyokuwa akisema ni kweli tupu. Eve aliamini na kutikisa kichwa kwa kuashiria kuwa alikuwa amemwelewa mgeni wake huyu.
“Eve nashukuru sana kwa yote uliyonitendea, ni imani yangu kuwa hakuna mtu ajuaye kuwa umenileta hapa. Au kuna mtu alikuona au anajua kuwa umenileta mahali hapa? Jacob aliuliza huku kayakaza macho yake usoni kwa Eve. Kabla ya kujibu Eve alisita na kuonyesha kuwa hakutegemea kupata swali kama hilo toka kwa Jacob.
“Hakuna mtu, lakini hata kama kungekuwa na mtu kwani kuna ubaya gani bwana Nico? Hatimaye Eve alisema katika hali ya kusita kidogo.
“Si unajua tena, wengine mabibi zetu wana wivu sana, wakipelekewa taarifa kuwa bwana wako kachukuliwa na msichana tena msichana mwenyewe mrembo kama wewe basi sidhani kama kutakuwa na amani huko nyumbani” Jacob alisema kwa utani uliokuwa umejaa uongo.
Ukweli ni kuwa Jacob hakuwa na hakika na sababu hasa ya wale watu waliomvizia kumpiga usiku ule kama walikuwa wanamfahamu au la. Alishindwa kuelewa ni nini kiliwafanya wao wakasirike yeye kuongea na yule mrembo Regina. Pia hakujua kwa nini Regina alikuwa kama mtu aliyeko kifingoni ili hali Tanzania ni nchi huru kabisa. Maswali mengi yalifumuka na ambayo mengine yalimpa wasiwasi.
“Nashukuru kwa kuwa hakuna aliyekuona, hivyo nina hakika ndoa yangu ni salama. Nafikiri wakati mwingine nikihitaji kuja kukutembelea hutakuwa na kizuizi chochote, maana sasa tu kama ndugu” Jacob alisema huku akiwa amekaa mkao wa kutaka kusimama. “Bila shaka ila mimi na wewe si kama ndugu bali ni marafiki sasa” Eve alijibu huku akicheka, bila shaka kauli ya Jacob ya uhusiano wa udugu hakuihafiki. “Basi bibie nitakuwa kama rafiki kwako. Sasa naomba uniruhusu niende nikaripoti kwa mama watoto juu ya wapi nilikuwa” Alisema akiwa anasimama. Macho ya Eve yalionyesha dhahiri kutoridhia na kuondoka kwa Jacob. Bila shaka alitaka kuwa na maongezi naye zaidi, japo hakujua ni nini wangeongea na Jacob. Alivutiwa na jinsi Jacob alivyoonekana kuwa mcheshi na mwelewa wa haraka. “Ningependa kujua nyumbani kwako ili wakati mwingine niwe namtembelea mama watoto wako. Au unaogopa inaweza kuwa vita? Eve alisema
“ Mke wangu ana wivu sana, lakini si kiasi cha kuogopa kutembelewa na watu wa jinsia yake. Bila shaka atafurahi sana kutembelewa na wewe. Kama ndivyo ipo siku nitakuja kukuchukua ili ukapafahamu nyumbani kwangu, bila shaka itakuwa vizuri” Jacob alisema hayo huku akiwa tayari kwa kuondoka.
*******
Wiki ilipita tangu pale Jacob alipopata mkasa ule pale hoteli ya Miami. Katika wiki yote hiyo hakuna siku ambayo hakwenda Miami Hoteli kwa lengo la kukutana na msichana Regina. Mara zote ambazo amekuwa akienda hakuna hata siku moja ambayo alifanikiwa kukutana na wala kumwona mrembo Regina. Jambo moja Jacob alilitambua ni kuwa Regina alikuwa na matatizo ambayo bila shaka yalihitaji kusaidiwa. Tatizo ni kuwa hakujua Regina alikuwa akiishi wapi na wala hawakuachiana njia yoyote ya mawasiliano.
Jumamosi hii nayo aliamua aende tena kujaribu bahati yake. Alifika Miami hoteli majira ya saa nne usiku, wakati ambao mambo yalikuwa yameanza kuchanganya sana ndani ya ukumbi wa hoteli. Kama nilivyosema awali, utulivu na umakini ni moja ya tabia ambazo Jacob alikuwa amejifunza. Kwa asili hakuwa amezaliwa hivyo, kwani alikuwa ni mtu mtundu na mdadisi wa kila linalopita mbele yake. Lakini kazi zake hizi za upelelezi zilimfundisha kuwa; utulivu na umakini ni moja ya silaha kali katika fani hii. Hili lilipelekea aanza kutafuta kwa bidii kuwa na tabia hizi. Alifanikiwa, kwa mtu yeyote aliyemfahamu Jacob alikiri kuwa alikuwa ni mtu mtulivu na makini. Hivyo alipoingia ukumbini hapo alitafuta sehemu iliyokuwa japo utulivu ili aweze kuwaona waingia na watokao na kusoma nyendo zao.
Alienda sehemu moja ambayo ilikuwa na watu walioonyesha kuwa walikuwa wa makamo kidogo kulinganisha na wengi waliokuwa ukumbini hapo. Aliagiza kinywaji laini na kuanza kunywa taratibu huku akijaribu kuangaza macho kama angeweza kumwona mtu wake - Regina.
Ilipofika saa sita kasoro hivi mara macho yake yakagongana na mtu ambaye sura yake haikuwa ngeni kwake. Jacob alimwangalia msichana huyo mpaka pale alipoenda kukaa. Msichana huyo alionekana kuwa peke yake. Alipokuwa amekaa aliagiza kinywaji. Macho ya Jacob hayakumwachia msichana huyo. Wakati fulani msichana huyo aligeuka na kuangalia upande ule aiokuwa amekaa Jacob. Alipomwona Jacob tu, msichana huyo alitabasamu. Ni tabasamu hilo ndilo lilomkumbusha Jacob kuwa msichana huyo alikuwa ndiyo yule Eve aliyemwokoa ukumbini hapo siku chache zilizokuwa zimepita. Jacob alikumbuka kuliona tabasamu hilo nyumbani kwa Eve muda mfupi tu mara baada ya yeye kulejewa na fahamu, Eve aliachia tabasamu la furaha kama hilo. Jacob alitabasamu pia kuitikia.
Eve alinyanyuka na kwenda pale alipokuwa amekaa Jacob. “Vipi umekuja na bibi yako” Alisema Eve katika sauti ya kunong’ona mara tu alipofika pale aliokuwa amekaa Jacob. Jacob hakujibu kitu bali alitabasamu tu. Hii ilidhihirisha kuwa Eve alikuwa ameamini asilimia mia kuwa Jacob alikuwa na mke kitu ambacho si kweli. Mpelelezi Jacob Matata hakuwa na mke, bali aliamua kumdanganya tu msichana huyo. “Karibu uketi na usiwe na wasiwasi” Hatimaye Jacob alisema na kumpa nafasi binti huyu aketi.
Jacob mara tu alipomwona Eve ndipo wazo la kumuhoji juu ya watu waliomchukua Regina siku ile ya tukio lilimjia. “Habari za tangu siku ile tulipoachana” Jacob alisaili
“Nzuri tu hofu kwako mgonjwa wangu, nimekuwa muuguzi mbaya asiyetaka kujua hali ya mgonjwa wake kwa kuacha kuja kukutakia hali” Alisema Eve huku macho yake akiyapepesa kiwizi wizi.
“Nadhani mimi ndiyo nimekuwa mkosefu zaidi kwa kuacha kuja kukujulia hali wewe mkombozi wangu” Jacob alisema huku akijaribu kuuusoma uso wa msichana huyu.
Baada ya salamu na utani wa hapa na pale Jacob na Eve wakajitoma katika kusakata muziki uliokuwa umepamba moto ukimbini hapo. Kila mmoja alijaribu kumwonyesha mwenzie kuwa alikuwa zaidi katika fani hiyo. Jacob kwa upande wake alikuwa na la zaidi, akili yake kwa upande mwingine ilikuwa ikimwaza msichana Regina na mkasa mzima uliokuwa umetokea. Mara kwa mara kwa chati alikuwa akiyazungusha macho yake karibuni ukumbi wote kuona kama angeweza kukutana na sura ya msichana yule aliyetoke kumvutia na wakati huo huo kugundua kuwa ni moja kati ya watu waliokuwa na matatizo yanayohitaji msaada wa mtu kama yeye. Kwa vyovyote vile, watu waliomchukua Regina si wema hata kama wanamfahamu. Ilikuwa wazi kichwani kwa Jacob kuwa watu walikuwa wanamfahamu na kuwa na uhusioano na Regina japo uhusiana wao yaonyesha haukuwa wa heri.
Hali ilipozidi kuwa mbaya kichwani, Jacob alimshika mkono Eve na kumvutia pembeni. ‘Samahani Eve kuna swali naomba nikuulize. Je waweza kuwa unawafahamu au kuwakumbuka watu walionifanyia uhuni ule siku ile hapa ukumbini ? Jacob alisema kwa sauti ya chini lakini kavu na ya baridi kiasi cha kuzigutua hisia za Eve. “Hapana, ila kama yule aliyekupiga kichwani akiletwa hapa naweza kumkumbuka” Eve alisema huku mikono yake akiipeleka kifuani kwa Jacob. Bila shaka alishahisi kuwa jambo lile bado lilikuwa linamsumbua Jacob. “Lakini maadamu u mzima, sioni sababu ya wewe kutaka kuwafuatilia maharamia kama wale. Cha msingi ilikuwa ni usalama wako. Kwani unafikiri ni kwa nini walikufanyia hivyo ? Hatimaye Eve aliuliza swali ambalo kwa muda alikuwa akishindwa namna ya kuanza kumwuliza Jacob. “Sijui hasa ni kwa nini, lakini nadhani ni kwa sababu ya yule msichana niliyekuwa nacheza naye” Jacob alisema huku akiziangalia mboni za macho ya Eve. “Ina maana yule msichana alikuwa bibi yao au ni wivu tu” Eve alitaka kujua zaidi
“Hapo ndipo sina uhakika. Mimi nilikutana naye humu humu ukumbini, nikamwomba tuwe naye na tucheze pamoja akakubali, japo alionyesha kuwa na wasiwasi kidogo” Jacob alijibu
“Kwa hiyo yawezekana wasiwasi wake ulitokana na kwamba alijua kuwa kucheza na kuwa na wewe ni makosa, kwa vile alikuwa na mtu ukumbini hapa ?
“Hilo sina hakika nalo sana ila kama ingetoke nikaonana naye angeweza kunieleza vizuri. Lakini tangu siku ile wamemchukua ukumbini hapa, sijamwona tena. Sijui nini kitakuwa kimemtokea au hajapata nafasi tu ya kuja tena” Jacob alisema huku akiachilia pumzi za kuonyesha kuwa jambo hilo lilikuwa likimtatiza.
Mara wote walishituliwa na tangazo la kuwaarifu kuwa muda wa kufunga ukumbi huo ulikuwa umewadia. Ilikuwa inaelekea kuwa saa saba za usiku. “Jacob mie nimekuja na gari yangu, hivyo kwa urahisi wa usafiri unaonaje kama tukaenda kulala nyumabni kwangu ? Sasa hivi taxi ni nadra sana na aghali mno, kwa usalama ni vema twende tu ukalale kwangu” Eve alisema huku akijifanya kutengeneza ukosi wa shati la Jacob.
“Hapana Eve kesho kuna sehemu nitatakiwa kuwahi sana kwa ajili ya biashara zangu, lakini iye pia nimekuja na gari langu” Jacob alikataa huku wakiwa wameanza kutoka ndani ya ukumbi huo. Kila mmoja alielekea alikojua.
***************************
Siku iliyofuata ilionekana kuwa ya ajabu ajabu tu kwa mpelelezi Jacob Matata. Sababu kuu kwa hili zingeweza kuwa nyingi, lakini iliyoonekana kuwa kubwa ni ile ya kufikilia suala la msichana aliyetokea kumpenda ghafula na ambaye ametoweka ghafula. Amempenda na katoweka Ghafula. Alionana na Regina kwa muda mfupi na kutokea kumpenda mara, lakini watu asiowajua walitokea, kumshambulia kwa sababu walizozijua wao, kumchukua msichana huyo aliyeoneka kuwa katika hali ya wasiwasi na ufungwa wa aina yake. Ingekuwa afadhali kwake Jacob kama watu hao hata wangemwachia Regina majeruhi kuliko kumchukua katika mzingira tata kama yale. Ilikuwa kama umeme kukatika wakati umeweka muvi uliyoitafuta kwa muda mrefu. Akili ya Jacob alitaka kujua undani wa Regina, lakini hakukuwa na mtu wa kumpa ukweli huo zaidi ya Regina mwenyewe, ambaye sasa hajui atampata vipi.
Mara nyingine Jacob alitaka kujilamu kwa kuchelewa kumwuliza Regina alikuwa akiishi wapi. Lakini wazo jingine likampinga kwa kuzingatia kuwa muda ulikuwa mfupi mno na ilikuwa mapema mno kwa hilo. Mara hisia za kupambana zilimji, zikamjaa, kawa tayari, akini hakuona wa kupambana naye. Alitafuta pa kuanzia kumtafuta Regina, hakupaona.
Mchana ilimkuta katikati ya jiji la Dar es salaam, hivyo chakula cha mchana akapata Steers. Ni wakati akiwa Steers anapata mlo wa mchana simu yake ya kiganjani iliunguruma, aliingalia kwa kukinaika, lakini alipoona jina la mpigaji kuwa ni Eve, aliinyakuwa mara moja. Eve ikimtaka Jacob nyumbani kwake haraka iwezekanavyo.
Jacob alijaribu kutafakari juu ya wito huo, alimwona Eve kama msichana aliyetokea kumpenda tu, kwa hivyo wenda alikuwa anataka aende ili akaongee naye tu. Kwa Jacob kupendwa na wasichana kama halikuwa jambo geni, kwani hata wakati akiwa shuleni walikuwa wakimgombani, yeyé alibaki akiwaangalia tu, maana hakujua walichokuwa wakikiona kwake na kukigombania. Hakuwa msafi, hakuwa na hela, wala hakuwa mzuri kama baadhi ya vijana wengine. Ni kweli alikuwa na kili darasani pamoja na utundu wake, lakini hakudhani kuwa hilo lingeweza kuwa sababu kubwa ya yeyé kugombewa na wasichana. Alipofika chuoni, pale chuo cha uhasibu Arusha hali ilkuwa hivyo hivyo, hadi baadi ya wanachuo wenzie wakadhani anatumia mizizi ya kwao Kigoma Umanyemani. Hakusita kuwapa walichotaka. Lakini kwa Eve alijikuta akisita kuwa karibu naye. Sababu hakuijua, ila wakati wa moja ya mafunzo yake huko china kuna mwalimu wake wa kichina alimwambia kuwa mara nyingine ni muhimu sana kama mpiganaji kuheshimu hisia zako.
Baada ya kujihoji na kujiuliza sana, hatimaye alijikuta akitia gari moto na kulitambaza taratiibu, ikulu, ocean road, daraja la salender huyo akaingia masaki, mtaa wa chake chake jirani na ofisi za Kilimanjaro International akasimamisha gari jirani na ilipokuwa nyumba ya Eve, ilikuwa ni saa nane na ushee mchana. Wakati kama huu jua la Dar es salaam lilikuwa likiwaadhibu wale wenzangu na miye wasiokuwa na namna ya kulidhibiti. Baada ya kuegesha gari eneo hilo alitembea taratiibu kuelekea geti la nyumba ya Eve. Ukubwa na uzuri wa nyumba ya msichana huyu ukilinganisha na kazi yake ya unesi ni moja ya vitu vilivyoacha maswali yasiyo na majibu kichwani mwa Jacob.
Alipofika getini, Jacob hakuchelewa kutambua kuwa kulikuwa na gari lililokuwa limeingia au kutoka mahali hapo muda mfupi uliopita. Alama za mataili na harufu ya mafuta ya gari bado vilikuwepo. Wakati anaiendea kengele ya getini hapo ili kuwajulisha wenyeji juu ya kuwepo kwake, alichungulia ndani na kuiona gari ya Eve ikiwa limeengeshwa. Hii ilionyesha kuwa si gari ya Eve iliyokuwa imetoka.
Muda mfupi tu mara baada ya kubonyeza kengele ya kutaka kufunguliwa geti, mlinzi alikuja na baada ya mahojiano alifunguliwa na kuelekezwa sehemu ambayo aliambiwa kuwa Eve alikuwa akimsubiri. Jacob kwa chati aliangaza macho yake hapa na pale hapo nje kabla ya kuingia sehemu aliyokuwa ameelekezwa.
“Ooh asante kwa kuitikia mwito wangu, karibu sana” Eve alisema kwa furaha huku akimkimbilia Jacob na kumkumbatia. Jacob hakuwa na namna ya kukataa bali kukubaliana na hali halisi. “Asante sana” alisema akiwa ameshikwa mkono na Eve kupelekwa sehemu ya maongezi.
“Utanisamehe kwa vile hatutakuwa na muda wa kuongea sana, huu ni wakati ambao natakiwa nielekee kazini. Lakini jambo lililonifanya nikuite haraka ni juu ya swali moja ulilokuwa umeniuliza jana, kama nilikuwa namfahamu mtu aliyekupiga na kuondoka na yule msichana Regina pale ukumbi wa hoteli ya Miami. Ni kwamba leo alikuja mzee mmoja ambaye tuko ofisi moja, alikuwa amekuja kwa masuala ya kikazi. Lakini alikuwa ameendeshwa na dareva mmoja ambaye mara alipoingia tu hapa niliweza kumtambua kuwa ndiye yule kijana aliyekushambulia siku ile na kumchukua Regina kwa kushirikiana na wenzie. Nilimwuliza yule mzee juu ya kijana huyo, akaniambia kuwa ni dereva wa shirika linalomiliki hospitali tunayofanyia kazi. Kweli nilishituka sana nilipomtambua” Macho ya Jacob yalipokuwa yakigongana na yale ya Eve Jacob alibaini kuwa msichana huyu hakuwa na hata chembe ya hila katika maelezo yake. “Je ulimwambia kuwa umemfananisha na lile tukio? Jacob alihoji
“Hapana sikutaka kumshitua haraka kiasi hicho” Eve alijibu
“Je waweza kuniandalia mazingira ya kuniwezesha kuonana na huyo dereva ?
“Hilo lisikupe shaka, leo hii nikienda kazini nitafanya kila mbinu ili uweze kumjua na huyo dereva”
“Ila naomba usijaribu kutaka kumuhoji kwa njia yoyote wala kumchunguza, sana sana ningependa kujua anaishi wapi na namba ya gari analoendesha” Jacob alisema
“sawa na……..” Kabla Eve hajamaliza alichotaka kusema mlio wa simu ulimzuia. Aliichukua simu yake ya mkononi na kupokea.
“sawa sasa hivi nakuja” Lilikuwa ni jibu la Eve mara baada ya kusikiliza kilichosemwa na upande wa pili wa simu hiyo. Aliposema hivyo alisimama haraka na kukimbilia chumbani. Alipotoka alikuwa tayari ameshavaa. “Samahani Jacob, kuna sehemu nahitajika haraka sana. Nadhani mambo mengine itakuwa kesho, nitakupigia ili uje nikupe nitakapokuwa nimefikia. Kwa sasa sina la ziada, labda tu nikupe lifti ili kukusogeza hapo Coco beach hotel pale waweza kupata usafiri kwa urahisi” Eve alisema huku akielekea chumbani kwake tena. Safari hii alipotoka tayari alikuwa ameshachukua mkoba wake na kuanza kuelekea ulipo mlango wa kutokea nje.
“Salama lakini uko uendako ? hatimaye Jacob aliona aulize mara baada ya kuona uharaka ule. “Salama tu” Eve alijibu huku tayari akiwa nje. Waliingia ndani ya gari, geti likafunguliwa ili kuwaruhusu kutoka. Jacob aliona alijikuta anashindwa kumwambia Eve kuwa alikuwa amekuja na gari lake. Mambo yalifanyika kwa haraka na alitaka ayaone jinsi yaendavyo.
“Kwa hiyo kesho nitakutaarifu nimefikia wapi, ila jiandae tu maana wakati wowote nitakuita” Eve alisema wakati alipokuwa amesimamisha gari ili Jacob ashuke tangu watoke naye nyumani kwake. Eve alikuwa na haraka ya kuwahi wito wa bosi wake. Jacob aliposhuka tu, Eve aliondoa gari kwa kasi ili kuwahi alikokuwa ameamuliwa kwenda kukutana na bosi wake.
“Nilikuwa nataka umsindikize mpenzi wako kisha turudi tukaongee vizuri nyumbani kwako, geuza gari turudi nyumbani kwako” Ghafula sauti ilisikika toka kiti cha nyuma, Eve akataka kugeuka ili aangalie msemaji ni nani lakini shingo yake ilipoguswa na kitu cha baridi alitulia tuli. Hakungoja kuambiwa kuwa kitu kilichomgusa ni bastola. Kwa chati aliyainua macho yake na kumwangali huyo mtu kupitia kioo cha mbele cha gari aliona kuwa sura ya jamaa huyu haikuwa na heri hata kidogo. Alipoangalia vizuri aliweza kumwona yule dereva ambaye muda si mrefu ametoka kumwambia Jacob kuwa ndiye aliyempiga na kitu kizito kule Miami hoteli, kijana huyo alikuwa ameshikilia bastola mkononi huku tabasamu la dhihaka likiwa usoni.
Hakuwa na hiari zaidi ya kufanya kama alivyokuwa ameelezwa. Mara moja picha ya msichana Regina ilimjia kichwani mwake, na kuanza kuwaza kuwa yaliyompata Regina yawezekana yakampata na yeye pia. Aliwaza na kuhisi kuwa yawezekana Jacob ana kitu kati yake na watu hawa. Alitamani kumpigia simu Jacob lakini alijua fika kuwa asingefanikiwa. Alipofika kwake alikuta gari mbili ndogo zikiwa zinapakia baadhi ya vitu vyake. Alipotaka kuhoji juu ya hilo, alizuiliwa na huyo kijana.
Wakati Eve anataka kuingia ndani, mara, simu yake ya mkononi iliita. “Hallow Nico, niko nyumbani wameni……” kabla hata hajamaliza alichotaka kusema alishitukia ananyang’anywa simu kwa nguvu. ‘Nani tena huyo jamani, niacheni basi angalau niongee na simu hivi nini hiki mnanifanyia ?!! Eve alilalamika.
*****
Ni sauti hii ya kulalamika ambayo ilimshitua Mpelelezi Jacob Matata aliyekuwa amepiga simu hiyo ili kumtaarifu Eve kuwa alikuwa amesahau funguo zakepale walipokuwa wamekaa. Sauti hii iliashiria kuwa msichana huyo alikuwa kwenye matatizo. Jacob alibonyeza tena namba za Eve na kupiga, lakini safari hii simu yake ilikuwa tayari imeshazimwa.
Kwa vile Jacob tayari alikuwa ameshakodisha gari kuelekea kwenye mizunguko yake, alimwamuru dereva aelekee nyumbani kwa Eve. “Haraka hebu nipeleke Sinza” Jacob alisema huku akipapasa kiunoni kwake ili kuona kama bastola yake ilikuwepo, alipoinona alitulia tuli na kumwachia dereva kazi yake.
Alipofika nyumbani kwa Eve tayari alikuwa ameshachelewa. ‘Shiit !!!!! Kuna namna tu hapa lazima kuna mchezo unafanyika tu. Wameanza na Regina na sasa Eve ? Jacob alijikuta akiropoka mwenyewe, na kumwacha dereva taxi aliyemleta mpaka hapa abaki anashangaa. “Kwani vipi kaka ? hatimaye yule dereva aliuliza.
“Huyu msichana mwenye nyumba hii namfahamu” Jacob alijibu huku akiwa anatoka ndani ya gari.
Baada ya kuuliza majirani hapo walimweleza kuwa inasemekana hakukuwa na mtu kabla ya moto kuzuka.
Hapo Jacob akajua kuwa Eve naye amechukuliwa kama alivyochukuliwa Regina. Hapo tena akataka kuanza kujilaumu kwa kuchelewa kumwuliza Eve alikuwa akifanya kazi wapi. Kila kitu ilikuwa kama harufu tu ibebwayo na upepo na kutoweka nao. Jacob aliachia pumzi ndefu na kujisemea ''kazi ipo!!!! Akatabasamu.....tabasamu la kukarahika. Ilikuwa yapata saa kumi na nusu jioni wakati Jacob alipoondoka eneo la tukio.
ITAENDELEA
0 MAONI :
Post a Comment